Loading...
http://go.ad2up.com/afu.php?id=778977

KIKAOA CHA RAIS MAGUFULI NA WABUNGE CCM CHAZUA SINTOFAHAMU ZITO WABUNGE WANENA MAZITO MNO.

Ikiwa ni takriban siku 40 baada ya kikao kizito kilichofanyika Ikulu ya Chamwino mjini Dodoma, wabunge wa CCM watakuwa na mkutano mwingine keshokutwa ulioitishwa na mwenyekiti wa chama hicho, Rais John Magufuli.

Hata hivyo, wabunge hawajaelezwa mahali wala muda utakaofanyika mkutano huo, kwa ahadi kuwa watataarifiwa baadaye.

Pia , wabunge hao hawajaelezwa ajenda za kikao hicho ambacho kwa kawaida huwa cha siri na ambacho hutumika kuweka misimamo ya chama katika masuala yanayojadiliwa au yanayotarajiwa kujadiliwa bungeni.

Katibu wa wabunge hao, Jasson Rweikiza ndiye aliyetuma ujumbe huo mfupi wa simu kwa wabunge ambao baadhi yao wameithibitishia Mwananchi suala hilo.

Ujumbe huo umemtaka kila mbunge awepo na hata wale waliosafiri, wajitahidi kurudi Dodoma kuhudhuria kikao hicho.

Alipohojiwa na gazeti hili jana, Rweikiza alisema Rais anaruhusiwa kuzungumza na wabunge wake muda wowote kwa hiyo hilo lisiwe nongwa linapotokea kwa CCM.

“Kwani (mwenyekiti wa Chadema, Freeman) Mbowe akiwataka wabunge wake inakuwa nongwa? Yeye ni mwenyekiti. Wabunge ni watu anaofanya nao kazi pamoja, hivyo kuwaita ili kuteta nao kujadili kazi isiwe nongwa,” alisema Rweikiza.

Rweikiza alisema Magufuli kama mwenyekiti wa CCM anaruhusiwa kuwaita wabunge na kukaa nao, kuongea au kuteta jambo lolote linalohusu mustakabali wa chama hicho.

“Mkumbuke yeye ni mwenyekiti wa chama tawala,” alisema.

Viongozi wa juu wa CCM na Serikali wanatarajiwa kuwepo katika kikao hicho, hasa kutokana na ukweli kuwa siku inayofuata itakuwa ni sherehe za Muungano ambazo mwaka huu zinafanyika mjini hapa.

Kwa maana hiyo, Rais Magufuli, Dk Ali Mohamed Shein (Rais wa Zanzibar), Samia Suluhu Hassan (Makamu wa Rais) na Phillip Mangula (makamu mwenyekiti CCM) na Abdulrahman Kinana (katibu mkuu wa CCM) wanatarajiwa kuhudhuria kikao hicho.

Vigogo hao wataungana na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa ambaye yupo mjini hapa kuongoza shughuli za Serikali bungeni.

Vikao hivyo huwa vinaongozwa na Waziri Mkuu katika siku za kawaida za mikutano ya Bunge kwa kuwa mtendaji huyo mkuu wa Serikali huwa Dodoma kwa ajili ya mikutano ya Bunge.

Mara ya mwisho kikao baina ya Rais na wabunge hapo kilifanyika Machi 12, mwaka huu na Rais alitumia muda mwingi wa hotuba yake kuwaelekeza wabunge jinsi ya kuenenda, ikiwa ni pamoja na kuwaonya wasimpinge Waziri Mkuu.

Maelekezo ya Rais

Katika kikao hicho ambacho pia kilihudhuriwa na Kinana na Mangula, kiongozi huyo wa nchi aliweka bayana kuwa iwapo wabunge watampigia kura ya kutokuwa na imani naye (Waziri Mkuu Majaliwa), atamrudisha kwenye chombo hicho na iwapo watamkataa tena, atalivunja Bunge.

Rais aliwaambia watunga sheria hao kutoka CCM kuwa amepata taarifa kwamba wapo baadhi yao wanaotishia kuanzisha hoja ya kutaka Majaliwa apigiwe kura ya kutokuwa na imani naye na kuwaambia wenye lengo hilo hawatafanikiwa kwa kuwa wakithubutu kufanya hivyo, atapeleka tena jina lake na wakirudia, atalivunja Bunge ili wote warudi katika uchaguzi.

Mbali ya kumkingia kifua Majaliwa, mwenyekiti huyo wa CCM pia aliwaonya wabunge dhidi ya vitendo vya kushirikiana na wapinzani kuishambulia Serikali, akitoa mfano wa mbunge wa chama tawala aliyemgawia muda wake wa kuchangia hoja mbunge wa upinzani.

Kwa kauli hiyo, alikuwa akirejea kitendo cha mbunge wa CCM, Boniface Getere kumpa dakika tano mbunge wa Serengeti (Chadema), Marwa Ryoba wakati wa kuchangia taarifa ya Kamati za Bunge za Ardhi, Maliasili, Kilimo na Utalii.

Pia alieleza kukerwa na wabunge wa CCM wanaofifisha vita dhidi ya dawa za kulevya na mmoja akimtuhumu kutoa siri za chama kwa upinzani.

Rais Magufuli pia alieleza kuwa yeye ndiye aliyeamua kusitisha matangazo ya moja kwa moja ya televisheni kwa baadhi ya shughuli za Bunge.

Pia, mwenyekiti huyo wa CCM alionya kitendo cha baadhi ya wabunge wa chama hicho waliotaka kumtembelea gerezani Arusha, mbunge wa Chadema, Godlbess Lema kwa madai kuwa kitendo hicho ilikuwa ni sawa na usaliti kwa chama.

Katika kikao hicho, wabunge pia walimweleza Rais kuhusu uhusiano wao na baadhi ya wakuu wa mikoa na wilaya, wakisema si mzuri na bado suala hilo limeendelea kujitokeza katika mijadala ya Bunge la Bajeti.

Baada ya kuwasikiliza, Rais Magufuli alianza kuwapa taarifa za mafanikio ya Serikali yake pamoja na mipango kabambe katika kutekeleza ilani ya uchaguzi ya CCM, akiwataka waiunge mkono Serikali katika maeneo yao huku suala la ujenzi wa reli pana, ambao tayari umezinduliwa, likipewa kipaumbele zaidi.

Kikao moto cha Bunge

Kikao cha keshokutwa kinakuja wakati Bunge likiwa limetawaliwa na mijadala inayoonyesha Serikali haijafanya kazi yake vizuri baada ya hotuba tatu za bajeti kusomwa.

Bajeti hizo ni ya Ofisi ya Waziri Mkuu, ambayo ilitawaliwa na majadiliano kuhusu vitendo vya utekaji, uvamizi na kuihusisha Idara ya Usalama wa Taifa na matukio hayo.

Suala la kutekwa kwa msanii Roma Mkatoliki, kitendo cha mteule wa Rais kuvamia studio za televisheni za Clouds Media, kutishiwa bastola kwa mbunge wa Mtama, Nape Nnauye na kutoweka kwa kada wa Chadema, Ben Saanane yalitawala mijadala ya hotuba hiyo.

Bajeti nyingine ni za Ofisi ya Rais (Tamisemi) na Utumishi wa Umma na Utawala Bora, zilizojadiliwa kwa pamoja na kutawaliwa pia na hoja za utekaji na pia vitendo vya unyanyasaji unaofanywa na wakuu wa wilaya na mikoa.

Mawaziri pekee watetea

Tofauti na inavyokuwa wakati wa bajeti hizo, ni wabunge wachache wa CCM waliosimama au kuomba mwongozo wakati wapinzani walipokuwa wakiishambulia Serikali.

Badala yake, mawaziri watatu; George Simbachawene (Tamisemi), Angela Kairuki (Utawala Bora) na Jenista Mhagama (Bunge) ndio waliosimama mara kwa mara kutoa taarifa au kuomba mwongozo.

Hoja dhidi ya Serikali zinazotolewa na wabunge wa upinzani pamoja na wa CCM zinaweza kuchukua nafasi kubwa katika kikao cha keshokutwa, hasa ikizingatiwa kuwa shughuli nyingi za maendeleo hazikupata fedha za kutosha kama ilivyopangwa katika bajeti iliyopita.

Hadi wiki mbili zilizopita, miradi ya maendeleo ilikuwa imepewa asilimia zisizozidi 40 ya fedha zilizotengwa. Bajeti ya mwaka 2016/17 ilitenga asilimia 40 ya fedha zake kwa ajili ya miradi ya maendeleo.

Bajeti hiyo ya mwaka 2016/17 ilikuwa ya Sh29.5 trilioni na Sh11.8 trilioni zilitengwa kwa ajili ya miradi ya maendeleo.

Wabunge wamekuwa wakiilalamikia Serikali kuwa fedha zinazotolewa kwa ajili ya shughuli mbalimbali haziendani na kiwango kilichoidhinishwa na Bunge hilo na kusababisha nakisi ya zaidi ya asilimia 50 katika miradi ya maendeleo.

Hali ya uchumi inaweza kuibua mijadala mikali katika hotuba za bajeti za wizara zinazofuata, kutokana na malalamiko kuzidi kuongezeka, hasa sekta binafsi ambayo wadau wanadai kuwa mazingira ya biashara hayajakuwa rafiki.

Suala jingine ambalo limekuwa linazungumzwa na wabunge kutoka vyama vyote ni uhakiki wa vyeti vya mteule mmoja wa rais anayedaiwa kufeli kidato cha nne na kutumia vyeti vya mtu mwingine ambavyo vimeghushiwa jina ili vilingane na jina lake la sasa.

Suala hilo pia lilihojiwa na wabunge wa CCM katika kikao chao cha kwanza cha ndaniokabla ya mkutano wa bajeti kilichoongozwa na Waziri Mkuu.

Vilevile, zimekuwapo taarifa za wabunge kutaka masilahi yao yaongezwe, lakini hoja zao zimekuwa zikigonga mwamba na taarifa za ndani zinasema safari hii huenda kilio chao kikaongezeka.

Bunge, ambalo mwaka jana lilirejesha salio la Sh6.5 bilioni, mwaka huu limejikuta na nakisi ya Sh8.5 bilioni ambazo wabunge wameeleza hofu kama zitaweza kukifikia chombo hicho kabla ya kumaliza shughuli zake za bajeti.

Post a Comment

CodeNirvana
Newer Posts Older Posts
© Copyright JAMIIYETU | Designed By BAKI NASI
Back To Top