Rais John Magufuli, amemtumia salamu za rambirambi Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini (IGP), Ernest Mangu, kufuatia kifo cha msaidizi wake, Inspekta Gerald Ryoba, aliyepoteza maisha pamoja na familia yake katika ajali ya kusombwa na mafuriko ya maji wakati akikatiza katika eneo la Kibaigwa, wilaya ya Kongwa, mkoani Dodoma.
Katika ajali hiyo iliyotokea Januari 3, mwaka huu, Inspekta Ryoba akiwa na mkewe na watoto wake wawili, pamoja na watu wengine wawili waliokuwa wakisafiri kutoka Geita kwenda Dar es Salaam, gari walilokuwa wakisafiria lilisombwa na maji na wote sita kupoteza maisha, katika eneo la Bwawani.
Katika salam zake za rambirambi alizomtuma, Rais Magufuli alimpa pole IGP Mangu kwa msiba huo mkubwa na amemuomba amfikishie salamu za pole kwa familia ya marehemu Ryoba na kueleza kwamba anaungana nayo katika kipindi hiki kigumu.
“Nimesikitishwa sana na tukio hili la kuondokewa na msadizi wako pamoja na familia yake, ni tukio linalotia uchungu mkubwa,” alisema na kuongeza:
“Namuomba Mwenyezi Mungu awape nguvu na uvumilivu wafiwa wote na aziweke roho za marehemu mahali pema peponi, amina.
CHANZO: NIPASHE


Post a Comment