Mkuu wa Nkoa wa Katavi, Dk. Ibrahim Msengi, amelitaka Jeshi la Polisi kuwa na uhusiano mzuri na wananchi ili kukabiliana na vitendo vya uvunjifu wa amani vinavyoendelea kuongezeka mkoani hapa.
Akizungumza katika sherehe za Siku ya Polisi mkoani Katavi katika katika ukumbi wa Katavi Resort mjni hapa, alisema uhusiano mzuri baina ya watendaji na wananchi ndiyo siri kubwa ya mafanikio.
Alisema kuwa hivi sasa vitendo vya uvunjaji sheria vinaongezeka licha ya kuwa polisi wanajitahidi kukabiliana navyo.
Mkuu wa mkoa alisema watu wa kwanza kujua mipango ya kufanyika uhalifu ni wananchi na kama kutakuwa na ushirikiano mzuri wananchi hao wanapaswa wawe wanatoa taarifa haraka.
Dk. Msengi alisema watu waovu wote wako kwenye jamii na wakati mwingine wananchi wanawajua kwa majina na hata wanapoishi. Kutokana na hali hiyo, alisema kinachotakiwa ni wananchi kwa kujengewa uwezo wa kutoa tarifa za siri ili iwe rahisi kukabiliana nao.
Pia alisema polisi wanapaswa kuwa na mbinu mpya za kukabiliana na wahalifu kwa kuwa uhalifu unabadilika kila siku na teknolojia inakua, hivyo ni vizuri nao wakaenda sambamba na wakati.
Aliongeza kuwa polisi ni jeshi linaloheshimika mkoani hapa hivyo ni lazima wawe waadilifu na nidhamu ya hali ya juu kwa kuwa wananchi wana imani nao kutokana na kuwa kimbilio lao wanapopatwa na matatizo ya kiusalama.
Kwaupande wake, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Katavi, Dhahiri Kidavashari, alisema pamoja na changamoto kubwa wanazokutana nazo, hawatakubali wahalifu waendelee kufanya wanavyotaka.
Aliongeza kuwa wamejipanga kumaliza wimbi la mauaji lililojitokeza hivi karibuni pamoja na kukabiliana na ujangili mkoani hapa.
CHANZO: NIPASHE


Post a Comment